Sunday, May 28, 2017

VIJANA TUJIONGEZE

    Tokeo la picha la YOUTH QUOTES ABOUT USING THEIR TIME
1.       Wakati umeshafika, Vijana tukaamka
Tuache kulalamika, Fursa tukazishika
Nguvu tunazo hakika, Tusiwe wa kubweteka
Akili zikatumika, Uchumi bora kuweka.

2.       Vikundi tukaviweka, Kwa umoja tutafika
Tukaenda nakufika, Majembe tukayashika
Kazi sera imefika, Shambani pakachimbika
Ajira zisipotoka, Akili huchangamka.

3.       Mvi hazijatufika, Muda nguvu tukaweka
Kazi tukashughulika, Fedha halali kushika,
Uvivu wa kuamka, Na mwilini kututoka
Vitanda tukavyondoka, Kulitupa nalo shuka.

4.     Tusome sana hakika, Kesho picha tukaweka
Ipo siku itafika, Chuoni tutaondoka
Mambo yakakamilika, Uzembe ukatuvuka.
Tusione tumefika, Vijana tukabweteka.

5.       Sisi tunahitajika, Jamii kuchakarika
Vipaji vikatumika, Na nyimbo zikaimbika
Vitabu tukaandika, Hazina kesho kuweka.
Vilevi mbali kuweka, Mwili wapata kuchoka.

6.     Nguvu nyingi kuziweka, Na kazi kumalizika
Mengine mwili wachoka, Safari kutoifika
Busara nazo kushika, Uzee tukaufika
Kwa Nguvu tunasifika, ni heri zikatumika.

7.       Kituo nimekifika, Nasaha kuzikumbuka
Mvi na zitatufika, Sisi tusipoamka
Muda utatuponyoka, Tusiweze kuushika
Tuache tu kutamka, Vitendo visofanyika. 

Raymond Nusura Mgen.
0766461571/0676559211
Mgeniraymond@yahoo.com/raymondpoet@yahoo.com
 Chuo Cha Kumbukumbu Hubert Kairuki

0 comments:

Post a Comment