1. Usichoke kusubiri, malenga nawakumbusha
Usichoke kutabiri, ya kesho bora maisha
Usiache tafakari, mambo kuyaimarisha
Uishi na watu shwari, furaha yawe maisha.
2. Endelea kupambana, iwe usiku mchana
Mazuri ukayanena, macho mazuri kuona
Kama u bado kijana, andaa nzuri hazina
Usishi mambo ya jana, leo kushindwa kuona.
3. Panda mbegu zile nzuri, iko siku utavuna
Kwanza kuota subiri, zitamea utavuna
Nawe kama u mshairi, vitunge vizuri vina
Usichoke kusubiri, mbegu ulopanda jana.
4 .Uzuri siku zaenda, masaa yanasogea
Anza maisha kupenda, vizuri kujiishia
Anasa kutozipenda, hukatisha yako nia
Hekima itakulinda, itakuongoza njia.
5.Siku ipo vitakuja, leo unavyojifanyia
Uzuri wakati huja, hata ukisubiria
Kutimiza yako haja, kujifunza kutulia
Jenga nzuri zile hoja, ijao kufurahia.
6. Malenga namalizia, subira yavuta heri
Usache
kung’ang’ania, moyo ule wa saburi
Utaipata na njia, usipoileta shari
Vina vimeniishia, mwisho nakata shauri.
Na Raymond Mgeni
0766461571/0676559211
Chuo Cha Kumbukumbu Hubert Kairuki
Mgeniraymond@yahoo.com/
raymondpoet@yahoo.com
0 comments:
Post a Comment